Serikali ya Tanzania kupitia bodi ya mikopo Heslb Walitangaza kuanza kutoa mikopo ya Elimu kwa wanafunzi wa ngazi ya Stashahada au Diploma Waliokidhi vigezo vya kupokea Mkopo huo ,Tumekuandalia makala hii kuorodhesha vigezo na Masharti ya kupata mkopo kwa ngazi ya stashahada.
Vigezo vya Kupata Mkopo Ngazi ya Diploma
Sheria na Kanuni za Bodi ya Mikopo zinaainisha sifa na vigezo vya jumla kwa
wanafunzi wanaohitaji mkopo baada ya kudahiliwa na vyuo vyenye ithibati. Mwombaji
atatakiwa kuwa na sifa zifuatazo:-
- Awe Mtanzania mwenye umri usiozidi miaka 27 wakati wa kuomba mkopo;
- Awe amedahiliwa katika taasisi ya elimu inayotoa elimu ya ngazi ya kati nchini;
- Awe amekamilisha na kuwasilisha maombi ya mkopo kupitia mfumo wa maombi ya mkopo (OLAMS);
- Asiwe na ajira au mkataba wa kazi serikalini au sekta binafsi unaompatia mshahara au kipato;
- Awe amehitimu elimu ya Kidato cha Nne (CSEE), Cheti (astashahada) au Kidato cha Sita (ACSEE) ndani ya miaka mitano; yaani kati ya mwaka 2020 hadi 2024.
- Kwa mwanafunzi anayeendelea na masomo ahakikishe matokeo yake yanayomwezesha kuendelea na masomo yametumwa Bodi, kupitia Afisa Mikopo/uongozi wa Chuo.
Hali ya Kijamii na Kiuchumi
- Uyatima; aliyefiwa na mzazi au wazazi
- Familia au kaya ya kipato duni inayofadhiliwa na Mifuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) au taasisi nyingine za kitaifa zinazotoa ufadhili kwa kaya zenye vipato duni;
- Ulemavu wa mwombaji au wazazi wake
Nyaraka Za Kuambatisha Wakati Wa Maombi Ya Mkopo
Zifuatazo ni nyaraka muhimu za kuambatisha kwenye maombi ya mkopo: –
- Cheti cha kuzaliwa kutoka mamlaka husika, ZCSRA kwa waombaji kutoka Zanzibar au Namba ya Uhakiki (verification number) kutoka RITA kwa waombaji kutoka Tanzania Bara;
- Vyeti vya vifo vya wazazi kuthibitisha uyatima kutoka mamlaka husika, ZCSRA kwa waombaji waliozaliwa Zanzibar au Namba ya Uhakiki (verification number) kutoka RITA kwa waombaji waliozaliwa Tanzania Bara;
- Barua kutoka RITA au ZCSRA kuthibitisha taarifa za kuzaliwa kwa waombaji waliozaliwa nje ya nchi. Kwa mwombaji ambaye mzazi wake amefariki nje ya nchi anapaswa kuwasilisha barua kutoka RITA au ZCSRA kuthibitisha taarifa za kifo.
- Fomu ya Kuthibitisha Ulemavu wa mwombaji au mzazi wake iliyoidhinishwa na Mganga Mkuu wa Wilaya (DMO) au Mganga Mkuu wa Mkoa (RMO);
- Namba ya kaya ya Mnufaika kutoka kwenye Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) kuthibitisha ufadhili wa kiuchumi alioupata mwombaji wakati wa elimu yake ya sekondari.
SOMA HII :Hatua kwa Hatua Jinsi Ya Kuomba Mkopo Wa Elimu Ya Juu HESLB
Jinsi Ya Kutuma Maombi Ya Mkopo Ngazi Ya Diploma
Mchakato wa kuomba mkopo wa HESLB kwa ngazi ya diploma ni rahisi na unafanyika mtandaoni. Hapa kuna hatua za kufuata:
- Maombi Mtandaoni: Maombi yote ya mkopo yatafanyika kupitia Mfumo wa Maombi na Usimamizi wa Mikopo (OLAMS). Waombaji wote wa mikopo wanakumbushwa kutumia namba ile ile ya Mtihani wa Kidato cha Nne iliyotumika wakati wa udahili.
- Ujazaji wa Fomu: Baada ya kuingia kwenye mfumo, jaza fomu ya maombi kwa usahihi na ukamilifu. Hakikisha unaambatanisha nyaraka zote zinazohitajika kama zilivyoainishwa katika mwongozo huu.
- Upakuaji na Saini: Baada ya kukamilisha maombi mtandaoni, pakua fomu za maombi na mikataba ya mkopo. Gonga mihuri sehemu husika, saini fomu, na ambatanisha nyaraka zinazohitajika.
- Uwasilishaji wa Fomu: Wasilisha kurasa zilizosainiwa (nambari 2 na 5) kwenye fomu ya maombi katika OLAMS.
- Malipo ya Ada ya Maombi: Lipia ada ya maombi ya mkopo ya shilingi elfu thelathini (TZS. 30,000.00) kwa namba ya kumbukumbu ya malipo utakayoipata katika mfumo. Unaweza kulipia kupitia benki au kwa mitandao ya simu.
UPANGAJI WA MIKOPO
Upangaji wa mikopo utazingatia vipaumbele vifuatavyo:-
(i) Mwanafunzi mwenye udahili kwenye programu za vipaumbele vya Taifa kama
zilivyofafanuliwa katika Kipengele cha 6 cha Mwongozo huu zitazingatiwa;
(ii) Ufaulu wa kitaaluma uliomuwezesha kudahiliwa kwa ajili ya elimu ya ngazi ya kati;
na
(iii) Hali ya kijamii kama ilivyofafanuliwa katika kipengele cha 3.2 cha mwongozo huu.