Kansa ya uume ni ugonjwa wa nadra lakini hatari unaoweza kuathiri wanaume, hasa wale wasiozingatia usafi wa sehemu za siri au walio katika hatari ya maambukizi ya virusi vya HPV (Human Papilloma Virus). Ugonjwa huu unaweza kuanza kama mabadiliko madogo kwenye ngozi ya uume lakini kuendelea hadi kuwa saratani kamili ikiwa hautatambuliwa mapema.
Kansa ya Uume ni Nini?
Kansa ya uume ni aina ya saratani inayojitokeza kwenye ngozi au tishu za ndani za uume. Saratani hii huanza kama kipele, uvimbe au mabadiliko ya rangi, na huweza kusambaa kwa kasi endapo haitagunduliwa mapema.
Kwa kawaida huathiri wanaume waliotimiza umri wa zaidi ya miaka 50, lakini inaweza kujitokeza hata kwa vijana, hasa wasiotohara na wanaopuuza usafi wa sehemu za siri.
Dalili za Kansa ya Uume
Hapa chini ni dalili zinazoweza kuashiria uwepo wa kansa ya uume. Zingatia kuwa sio kila dalili ni kansa, lakini dalili hizi zinahitaji uchunguzi wa haraka.
1. Uvime au uvimbe kwenye uume
Mara nyingi hujitokeza kama uvimbe mdogo usio na maumivu
Hukua polepole au haraka
2. Vidonda visivyopona
Vidonda vinavyodumu kwa wiki kadhaa bila kupona
Huweza kuwa na usaha au damu
3. Kutoa uchafu au harufu mbaya kutoka kwenye uume
Uchafu mzito wenye harufu mbaya kutoka chini ya ngozi ya uume (kwa wasio tohara)
4. Mabadiliko ya ngozi ya uume
Mabadiliko ya rangi ya ngozi (kawaida kuwa nyekundu, kijivu au nyeusi)
Ngozi kuwa kavu au kupasuka
5. Kuwasha au kuungua kwenye uume
Kuwasha isiyo ya kawaida au kuhisi moto ndani ya uume au kwenye kichwa cha uume
6. Kuvimba kwa tezi kwenye kinena
Tezi zilizovimba upande wa kinena (nyonga) zinaweza kuwa ishara ya kansa inayosambaa
7. Maumivu wakati wa kukojoa au kujamiiana
Dalili hizi huonekana kwenye hatua za mbele za kansa
Sababu za Hatari Zinazochangia Kansa ya Uume
Kutokufanyiwa tohara (hasa kama usafi wa chini ya ngozi ya uume hautunzwi)
Maambukizi ya HPV (Human Papilloma Virus)
Kutumia sigara au tumbaku
Historia ya ugonjwa wa kansa kwenye familia
Kinga ya mwili iliyo chini (kama kwa watu wanaoishi na VVU)
Kutokufanya usafi wa uume mara kwa mara
Jinsi ya Kutambua Tofauti kati ya Kansa na Maambukizi ya Kawaida
Dalili | Maambukizi ya kawaida | Kansa ya Uume |
---|---|---|
Vidonda | Hupungua kwa dawa | Hudumu kwa muda mrefu, haviponi |
Harufu | Hutokana na fangasi au bakteria | Mara nyingi ni ya kudumu na huambatana na vidonda |
Upele | Hupona haraka kwa krimu | Upele wa kansa hubadilika kuwa uvimbe |
Maumivu | Mara chache | Huongezeka kadri muda unavyoenda |
Hatua za Kuchukua Unapoona Dalili
Usihofie – chukua hatua
Hata kama siyo kansa, usichelewe kupata msaada
Tembelea kituo cha afya au hospitali kubwa
Daktari atafanya uchunguzi wa macho, vipimo vya damu au kuchukua sampuli (biopsy)
Usitibu mwenyewe kwa dawa za dukani
Kuchelewa kupata matibabu huongeza hatari ya kansa kusambaa
Fanya uchunguzi wa mara kwa mara kama uko kwenye hatari kubwa
Mfano: ikiwa hujafanyiwa tohara, una VVU, au unatumia tumbaku
Namna ya Kujikinga na Kansa ya Uume
Fanyiwa tohara mapema (hasa utotoni au ujana)
Fanya usafi wa uume kila siku, hasa kwa waliotahiriwa na waliotoholewa
Epuka ngono zembe – tumia kondomu na pima mara kwa mara
Pata chanjo ya HPV (hasa kwa vijana)
Acha matumizi ya tumbaku na sigara
Epuka kujikuna au kutumia bidhaa za kemikali kwenye uume
Maswali Yanayoulizwa Mara kwa Mara (FAQs)
Ni kila kipele kwenye uume ni kansa?
Hapana. Vipele vingi ni vya kawaida au vya maambukizi ya ngozi au zinaa, lakini ikiwa haviponi, tafuta msaada wa daktari.
Kansa ya uume huwapata wanaume wa rika gani?
Mara nyingi huwapata wanaume wa miaka 50 na kuendelea, lakini huweza kutokea kwa vijana pia.
Je, kansa ya uume hutibika?
Ndiyo. Ikitambuliwa mapema, inaweza kutibiwa kabisa kwa upasuaji, mionzi au dawa za saratani.
Je, tohara hupunguza uwezekano wa kansa ya uume?
Ndiyo. Tohara mapema hupunguza hatari kwa kiasi kikubwa kwa kusaidia usafi wa uume.
Kuna uhusiano kati ya VVU na kansa ya uume?
Ndiyo. VVU hupunguza kinga ya mwili na hivyo kuongeza hatari ya kupata kansa, pamoja na magonjwa mengine.